Chelsea Yamsajili Tosin Adarabioyo Kutoka Fulham kwa Mkataba wa Miaka 4.

Beki Mpya wa Kilabu ya Chelsea Tosin Adarabioyo. Picha: Chelsea Fc

Klabu ya Chelsea imethibitisha kukamilisha usajili wa beki Tosin Adarabioyo kutoka Fulham kwa mkataba wa miaka minne. Chelsea, ambayo inatafuta kuimarisha kikosi chao, imemtangaza Adarabioyo, mwenye umri wa miaka 26, kama usajili wao wa kwanza katika dirisha hili la uhamisho, kwa uhamisho wa bila malipo.

Adarabioyo alikamilisha vipimo vya afya mapema wiki hii na anatarajiwa kujiunga na kikosi cha Chelsea katika Uwanja wa Stamford Bridge mwishoni mwa mwezi huu, mara tu mkataba wake na Fulham utakapoisha rasmi.

The Blues wametoa taarifa rasmi kwenye mtandao wao wa X wakidhibitisha usajili wa beki huyu, huku dirisha la uhamisho la Ligi ya Premia likitarajiwa kufunguliwa tarehe 14 mwezi huu. Usajili huu umekuja wakati mwafaka kwa Chelsea ambao wanatarajia kufanya mabadiliko makubwa kwenye kikosi chao kwa ajili ya msimu ujao.

Beki huyo, ambaye ni raia wa Uingereza, alikataa ofa kadhaa za kusaini kandarasi mpya katika kilabu ya Fulham katika Uwanja wa Craven Cottage, kabla ya kukubali kuwa mchezaji wa kwanza kusajiliwa chini ya kocha mpya wa Chelsea, Enzo Maresca.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *