Waziri Ababu Namwamba Aitaka Gor Mahia Kujiandaa Mapema kwa Mechi za CAF.

Mabingwa wa FKF PL Gor Mahia

Waziri wa Michezo Ababu Namwamba, ametoa wito kwa Gor Mahia kujitayarisha mapema kwa mechi za Kilabu bingwa barani Afrika. Waziri Namwamba amesisitiza matayarisho haya ili Gor Mahia wafanikishe safari yao baada ya kufungiwa nje ya michuano ya CAF mwaka jana.

Gor Mahia, ambao walinyakua taji lao la 21 la Ligi Kuu ya Kenya baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Muhoroni wikendi iliyopita, wanatarajiwa kuipeperusha bendera ya taifa katika mashindano ya Klabu Bingwa Afrika. Kogalo, kama wanavyofahamika, walishindwa kushiriki kwenye Makala ya mwaka jana baada ya kukosa kufikia vigezo vilivyowekwa na CAF kwa vilabu vinavyotaka kushiriki kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa.

Mwaka jana, Gor Mahia walifaa kuwakilisha taifa kwenye michuano hiyo, lakini suala la malipo ya wachezaji wao wa zamani, wakiwemo Adama Keita, Jules Ulimwengu, na Sando Yangayay, liliwafanya kutemwa nje licha ya juhudi za Shirikisho la Soka la Kenya (FKF), Wizara ya Michezo, na Waziri wa ICT, Eliud Owalo, kutaka kuwawezesha kurejea kwenye michuano hiyo.

Gor Mahia aidha wana afueni kwani wanatarajiwa kupokea mtaji mzito kutoka kwa usimamizi wa Ligi Kuu ya Kenya baada ya kutwaa ubingwa. Hii inatokana na mfadhili mpya wa ligi ambaye amekuwa akipeperusha mechi za ligi kuu msimu huu.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *